Thursday, November 8, 2012

Tuhuma za mabilioni yaliyofichwa Uswisi zatikisa nchi

                                        Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema)

MJADALA mkali uliibuka bungeni jana baada ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) kuwalipua baadhi ya viongozi waandamizi wa Serikali akitaka wachunguzwe kwa makosa ya kuficha mabilioni ya fedha nje ya nchi
Zitto alitoa kauli hiyo jana bungeni wakati akiwasilisha hoja yake binafsi kuhusu kulitaka Bunge kuchunguza na kuielekeza Serikali kuchukua hatua dhidi ya raia wa Tanzania walioficha fedha na mali haramu nje ya nchi.



Bila ya kuwataja kwa majina, mbunge huyo aliwataja watu hao kwa nyadhifa kuwa ni watu wote walioshika nyadhifa za uwaziri mkuu katika kipindi cha 2003 hadi 2010, walioshika nyadhifa za uwaziri wa nishati na madini katika kipindi hicho na waliokuwa makatibu wakuu Wizara ya Nishati na Madini.
Wengine ni mawaziri na makatibu wakuu wa Wizara ya Ulinzi, wakuu wa majeshi, wanasheria wa Serikali, makamishna wa nishati, walioshika wadhifa wa Ukurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Uenyekiti na Ujumbe wa Bodi wa TPDC katika kipindi cha mwaka 2003 hadi 2010.
Kutokana na hilo, Zitto aliitaka Serikali kupeleka bungeni muswada wa sheria bungeni wakati wa Mkutano wa 11 wa Bunge wa Aprili mwakani.

“Mbali na hilo napendekeza kuwa iwe ni marufuku kwa kiongozi yeyote wa umma au mume au mke wake au mtoto wake kuwa na akaunti nje ya nchi isipokuwa kwa sababu maalumu na kwa kibali rasmi kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano,” alisema Zitto
Pia Zitto alitaka Serikali kuwasiliana na Benki ya Dunia kupitia kitengo cha ‘Assets Recovery Unit’ ili mabilioni ya fedha na mali ambazo zimetoroshwa nje ya nchi kwenda Uswisi, Dubai, Mauritus na maeneo mengine ziweze kurejeshwa.
Aliwataka Watanzania wote wenye akaunti za fedha nje ya nchi waeleze wamezipata wapi na Takukuru wachukue hatua za kisheria dhidi ya watu wote wanaomiliki fedha hizo kinyume cha sheria.


No comments:

Post a Comment